Mathayo 19 : 29
Na
kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume au wa kike, au baba, au
mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara
mia, na kuurithi uzima wa milele.
Fundisho: “Tumeacha Vitu Vyote na Kukufuata Wewe”
Ili kutimiza daraka alilopewa duniani, Yesu “alijiondolea mwenyewe hali
yake na kuchukua umbo la mtumwa,” na hivyo kuacha maisha na utukufu
aliokuwa nao mbinguni. (Flp. 2:7)
Hata tukimwiga Kristo kadiri gani, yale tunayofanya hayawezi
kulinganishwa na yale ambayo Yesu alifanya alipokuja duniani. Lakini
tunaweza kubaki imara tukiwa wafuasi wake, kwa kutotamani mambo
tuliyoacha katika ulimwengu wa Shetani.—1 Yoh. 5:19.
Pindi moja, mtume Petro alimwambia Yesu hivi: “Tazama! Tumeacha vitu vyote na kukufuata wewe.” (Mt. 19:27)
Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana waliacha haraka nyavu zao walipoalikwa
wamfuate Yesu. Waliacha kazi yao ya uvuvi na kufanya huduma kuwa kazi
yao kuu. Kulingana na simulizi la Injili ya Luka, Petro alisema hivi:
“Tazama! Tumeacha vitu vyetu wenyewe na kukufuata wewe.” (Luka 18:28) Wengi wetu hatukuacha “vitu vyetu” vyote
ili kumfuata Yesu. Hata hivyo, tulihitaji ‘kujikana wenyewe’ ili kuwa
wafuasi wa Kristo na watumishi wa Yehova wenye kujitoa kwa moyo wote. (Mt. 16:24) Hatua hiyo imetuletea baraka nyingi. (Soma Mathayo 19:29.)
Kuwa na roho ya kueneza-injili kwa kumwiga Kristo kunaleta shangwe
moyoni mwetu, hasa ikiwa tumeshiriki hata kwa kadiri ndogo kumsaidia mtu
fulani amkaribie Mungu na Mwana wake mpendwa.
Valmir, Mbrazili anayeishi nchini Suriname, alikuwa mchimba-dhahabu.
Alikuwa mlevi na aliishi maisha mapotovu kiadili. Pindi moja alipokuwa
katika jiji fulani, Mashahidi wa Yehova walianza kujifunza Biblia pamoja
naye. Alijifunza kila siku, akafanya mabadiliko makubwa, na muda si
muda akabatizwa. Alipoona kwamba kazi yake inamtatiza kuishi kulingana
na mafundisho ya Biblia, aliuza biashara yake iliyokuwa yenye faida
kubwa naye akarudi Brazili ili kusaidia familia yake kupata hazina za
kiroho. Baada ya kujifunza kweli ya Biblia, wahamiaji wengi wanaacha kwa
kupenda kazi zao katika nchi zenye utajiri na kurudi katika nchi za
kwao ili kuwasaidia kiroho watu wao wa ukoo na wengineo. Kwa kweli,
wahubiri hao wa Ufalme wanaonyesha roho ya kueneza-injili.
Mashahidi wengi wamehamia katika maeneo ambako kuna uhitaji mkubwa
zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Wengine hata wanatumikia katika nchi za
kigeni. Huenda sisi binafsi tusiweze kuhama, lakini tunaweza kumwiga
Yesu kwa kufanya sikuzote yote tuwezayo katika huduma.
No comments:
Post a Comment