AGAPE SINGERS

Katiba











THE SEVENTH-DAY ADVENTIST CHURCH
MARA CONFERENCE


AGAPE GOSPEL SINGERS-MUSOMA 2013




KATIBA


TOLEO I
[Katiba hii imeandaliwa ili kulinda mfumo mzima wa kiutendaji wa kikundi]




SEHEMU YA I

KUHUSU KIKUNDI

  1. JINA
Jina rasmi la Kikundi litakuwa Agape Gospel Singers (AGS) 2013. Jina hili litatumika katika shughuli zote rasmi za kikundi, kanisa, mialiko na katika matangazo mbalimbali.

  1. ANUANI
Kikundi kitakuwa na Ofisi katika Manispaa ya Musoma-Mtaa wa Kamnyonge. Anuani itakakuwa:
 Agape Gospel Singers,
S.L.P 301
 MUSOMA.
 Barua pepe:   agsmusoma2013@gmail.com
Tovuti/Blog:    AGAPE GOSPEL SINGERS-MUSOMA

  1. MOTO
PIGA MBIU TANGAZA MAREJEO YA YESU KRISTO ULIMWENGUNI KOTE

  1. MAONO
Kwaya ya AGS inalenga kutoa fursa za kujifunza na kutoa huduma ya neno la Mungu kwa kuburudisha na kuelimisha kupitia nyimbo za ibada na matamasha. Ili kujitangaza na kujitanua ndani na nje ya mipaka ya Mara Conference na Union, wanakikundi watatazamiwa kutimiza wajibu wao wa kuhubiri kupitia muziki na kutenda kama mabalozi wema wa Yesu Kristo ndani na nje ya kanisa.

  1. MWONGOZO
Kikundi kimedhamiria kuwasaidia wanakwaya kujifunza muziki wa injili ili kuwawezesha kuwa waimbaji wa viwango vya juu, kuwa wataalam wenye ujuzi wa kufundisha muziki, waweze kujiajiri kupitia muziki na hivyo kusaidia maendeleo ya kanisa na ya jamii.



SEHEMU YA II

IMANI YA KIKUNDI

  1. MISINGI YA IMANI
Misingi ya Imani ya kikundi inajibainisha katika mambo yafuatayo:
Tunaamini katika:
1.      Nguvu na uweza wa Bwana wetu Yesu Kristo.
2.      Upekee, ukamilifu, ukweli na mamlaka ya Biblia Takatifu.
3.      Ulazima na uwezo wa ufufuo wa matumaini mapya unaotokana na kifo cha Yesu Kristo msalabani kwa ajili ya kuuokoa ulimwengu.
4.      Uwepo wa nguvu ya Roho Mtakatifu kwa kazi ya matengenezo na uumbaji mpya.
5.      Matumaini ya kurudi kwa Bwana wetu Yesu Kristo kwa ajili ya ufufuo na uzima wa milele.
6.      Uwezo na karama ya uimbaji kutoka kwa Mungu Baba kwa ajili ya kueneza injili ya Bwana wetu Yesu Kristo.

  1. MATARAJIO
Kikundi kina matarajio makubwa kwamba, kwa umuhimu wa kipekee, viongozi wote wa kuchaguliwa na kuteuliwa wa kikundi, wanachama na vikundi, watu binafsi au makampuni watakaoalikwa kwa ajili ya kuchangia kama njia ya kutimiza maono ya kikundi, bila ya kufungwa na misingi ya imani hapo juu, watajitoa kwa moyo kwa kadri Mungu alivyowajalia.





SEHEMU YA III

MALENGO YA KIKUNDI


  1. MALENGO YA MSINGI
1.      Kushuhudia kwamba Yesu Kristo ni Mungu halisi, na kujifunza kuwaongoza wengine kuamini kuwa Yesu ni Bwana na Mwokozi wetu. Lengo hili linatimizwa kupitia nyimbo na mawasiliano.
2.      Kuwasaidia wakristo kukua katika imani kama wanafunzi wa Yesu na kuwafundisha kuliona kanisa kuwa ni nyumbani kwao, kwa kusoma na kujifunza Biblia, kwa maombi na ushirika wa Yesu Kristo.
3.      Kuonyesha mwito wa Mungu kwa wanadamu kupitia maono ya kanisa.

  1. MALENGO YA ZIADA
1.      Kuhamasisha juu ya maendeleo ya elimu ya kiroho na mafunzo ya fani ya muziki.
2.      Kufanya mahubiri ya hadhara ili kuongoa roho nyingi kupitia nyimbo.
3.      Kuwatia moyo waliokata tamaa ya maisha kupitia nyimbo za injili ya Yesu Kristo.
4.      Kutumia mapato ya kikundi kufungua miradi mbalibali ili kutoa ajira kama sehemu ya mkakati wa kuvuta na kuwaleta kanisani.

  1. MAHITAJI
1.      Vifaa toshelevu vya kisasa vya muziki vinavyokidhi mahitaji ya kwaya.
2.      Usafiri wa kwaya.
3.      Jengo la ofisi ya kikundi.




SEHEMU YA IV

UANACHAMA NA USHIRIKA

Uanachama wa AGS upo wazi kwa jamii ya washirika wa kanisa la Wa-adventista wa Kisabato wa makanisa yaliyopo ndani ya Manispaa ya Musoma. Mwanachama atakuwa yule atakayeafikiana na matakwa ya sehemu ya II A na B ya katiba hii. Mwanachama atakuwa yule aliyejaza fomu ya maombi ya uanachama na kuthibitishwa au kupitishwa na bodi ya wakurugenzi ya kikundi kwa kukidhi vigezo vyote vitakavyopangwa na mkutano mkuu wa kikundi.
 
  1. AINA ZA UANACHAMA.
1.   WANACHAMA WAANZILISHI

Hawa ni wanachama waliobuni wazo na kuamua kuanzisha kikundi. Ni waanzilishi walioweka misingi, taratibu na kuandaa mipango yote ya kikundi.

2.   WANACHAMA WAPYA

Hawa ni wanachama walioomba na kukubaliwa kujiunga na kikundi baada ya kufuata taratibu na kutimiza vigezo vyote vya uanachama kwa mujibu wa katiba.

3.   WANACHAMA WATEULIWA

Hawa ni wanachama waliopendekezwa kutokana na fursa zao kwa ajili ya kukisaidia kikundi. Wamepewa uanachama kutokana na taaluma na au ujuzi walionao.

  1. SIFA, HAKI NA WAJIBU WA MWANACHAMA
1.   SIFA

                                                        i.            Mwanachama wa kikundi atakuwa M-Adventista M-Sabato mwenye ushirika katika kanisa lake anakosali.
                                                      ii.            Awe na akili timamu na awe na umri kuanzia miaka 18 na kuendelea.
                                                    iii.            Ajue kusoma na kuandika.

2.   HAKI

                                                        i.            Kila mwanachama atakuwa huru kutoa mawazo yake sahihi ndani ya kikundi
                                                      ii.            Kila mwanachama atakuwa na haki ya kusikilizwa na kusikiliza mawazo ya wenzake kwa upendo na unyenyekevu.
                                                    iii.            Kila mwanachama atakuwa na haki ya kuchagua au kuchaguliwa kuwa kiongozi wa kikundi.
                                                     iv.            Ni haki ya mwanachama kutoa taarifa sahihi kwa mtu sahihi na kwa wakati sahihi juu ya matumizi mabaya ya madaraka, ubadhirifu wa raslimali ya kikundi na matendo yote yasiyomtukuza Mungu miongoni mwa wanakikundi.
                                                       v.            Ni haki ya mwanachama kuhudhuria matamasha ya injili na mialiko mbalimbali inayohusiana na shughuli za kikundi.

3.   WAJIBU

                                                        i.            Kila mwanachama ana wajibu wa kuhudhuruia vikao na mikutano inayomhusu kwa nafasi yake katika kikundi.
                                                      ii.            Ni wajibu kwa kila mwanachama kufika kwa wakati na kushiriki kwa ukamilifu mazoezi yote ya kwaya.
                                                    iii.            Ni wajibu wa mwanachama-mwanakwaya kuwa na sare zote za kwaya zinazotakiwa kwa wakati na katika mazingira muafaka.
                                                     iv.            Kila mwanachama anawajibika kutekeleza kwa ufanisi na kwa wakati majukumu yake yote atakayopangiwa na kikundi.
                                                       v.            Ni wajibu wa kila mwanachama kulipa kiingilio, ada na michango yote stahiki  kwa kadri itakavyokuwa inaamriwa na vikao halali vya kikundi.




SEHEMU YA V

UONGOZI NA MAJUKUMU

  1. MKURUGENZI MKUU
1.      Atakuwa kiongozi mkuu wa kikundi.
2.      Atasimamia shughuli zote za AGS ikiwa ni pamoja na masuala ya imani, utawala, mipango, vikao, uchumi, mahusiano na mawasiliano, matangazo, raslimali, na usimamizi watovuti ya kwaya.
3.      Atawapangia majukumu viongozi na wanachama wengine na atakuwa kiungo muhimu kati ya wanakwaya na viongozi wa kikundi.
4.      Atahudumu kama mwenyekiti wa vikao vyote vya bodi ya wakurugenzi na mkutano mkuu wa kikundi.
5.      Ataratibu na kusimamia mialiko na safari zote za kikundi ndani na nje ya Manispaa ya Musoma.
6.      Atashauriana na bodi ya wakurugenzi kufanya uteuzi wa wataalamu muhimu wanaohitajika kuimarisha shughuli za kikundi.
  1. KAIMU MKURUGENZI MKUU
1.      Atasaidia na kusimama kwa nafasi ya Mkurugenzi Mkuu pale asipokuwepo
2.      Atahudumu kama msimamizi mkuu wa shughuli zote za matangazo na machapisho kwenye majarida, mitandao, vipeperushi n.k.
3.      Atahusika na ubunifu, uandaaji na ugawaji wa sare za kwaya.
4.      Atawajibika kwa majukumu mengine kwa kadri atakavyopangiwa na Mkurugenzi Mkuu.
  1. KATIBU MTENDAJI
1.      Atawajibika kuchukua na kuandaa taarifa ya mahudhurio ya vikao, mazoezi ya kwaya na matukio mengine ya wanachama.
2.      Ataandaa na kutunza taarifa na mihtasari yote ya vikao vyote vya bodi ya wakurugenzi na mkutano mkuu.
3.      Ataandaa ripoti zote za kikundi zinazotarajiwa kutumwa au kusambazwa kwa taasisi, watu binafsi au makampuni yenye mahusiano na kikundi.
4.      Atawajibika kwa majukumu mengine atakayopangiwa na Mkurugenzi Mkuu. Iwapo atapata udhuru wa mahudhurio ya kikao, nafasi yake itakahimiwa na mwanachama yeyote miongoni mwa wajumbe wa bodi ya wakurugenzi.
  1. MKURUGENZI WA UCHUMI NA FEDHA
1.      Ataandaa bajeti ya mwaka ya kikundi kwa kushirikiana na bodi ya wakurugenzi.
2.      Atawajibika kuandaa na kutolea taarifa kwa wakati matumizi yote ya fedha yaliyopangwa kutumiwa na kwaya katika shughuli zake za kila siku.
3.      Atapokea na kuhakikisha anatunza kwa usahihi mapato yote yatokanayo na michango na makusanyo yote ya kikundi kutoka vyanzo mbalimbali.
4.      Atawajibika kwa majukumu mengine ya kikundi kwa kadri atakavyopangiwa na Mkurugenzi Mkuu.
  1. MKURUGENZI WA MAKTABA NA MAWASILIANO
1.      Atakuwa mwangalizi na msimamizi mkuu wa maktaba ya kwaya.
2.      Ataandaa na kutunza vifaa vyote vya muziki na mafaili yote (Kanda na CD’s).
3.      Atatunza na kuifanyia marekesho tovuti ya kikundi na kuhakikisha pia anaiwekea taarifa zote stahiki. Atakuwa chini ya uratibu wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu.
4.      Ataandaa na kutunza taarifa zote za machapisho, picha na sare zote za kwaya.
5.      Atapokea na kutoa taarifa zote ndani na nje ya kikundi.
6.      Atawajibika kwa majukumu mengine ya kikundi kama atakavyopangiwa na Mkurugenzi Mkuu.
  1. MKURUGENZI WA MUZIKI NA MAHUSIANO
1.      Atashirikiana na wasaidizi wake kuongoza kwaya katika shughuli zote zinazohusu muziki na kufanya uteuzi wa nyimbo kwa ajili ya Ibada na matamasha ya injili.
2.      Atashirikiana na wataalamu wa ndani na nje ya kikundi kutunga na kufundisha nyimbo katika kwaya na kuratibu matumizi ya majukwaa na kurekodi nyimbo.
3.      Yeye na wasaidizi wake watatoa ushauri na mapendekezo juu ya muundo wa kwaya na kuwa kiungo muhimu kati ya mwanakwaya mmoja mmoja na kikundi.
4.      Atasikiliza na kutolea ushauri shida na matatizo mbalimbali ya wanakwaya.
5.      Atawajibika kwa majukumu mengine atakayopangiwa na Mkurugenzi Mkuu. Bodi ya wakurugenzi itateua mkurugenzi mpya kuchukua nafasi wazi itakayoachwa na mkurugenzi wa kwaya kwa sababu yoyote ile.



SEHEMU YA VI

VIKAO NA MAJUKUMU

Kikundi kitaendesha shughuli zake kwa mujibu wa vikao halali vya wanachama. Kutakuwa na vikao vya aina kuu tatu: Mkutano mkuu, Bodi ya wakurugenzi na Baraza la  wadhamini. Kila mwanachama anatarajiwa kuhudhuria vikao vyote vinavyomhusu kwa mujibu wa katiba. Mwanachama atakayekosa vikao vitatu (3) na ama mazoezi ya kwaya mfululizo pasipo  taarifa rasmi atachukuliwa hatua ya kinidhamu kwa kadri itakavyoamriwa na bodi ya wakurugenzi.

  1. MKUTANO MKUU
1.      Mkutano mkuu ndicho kikao kikuu cha wanachama wote.
2.      Mkutano mkuu utafanyika mara mbili (2) kwa mwaka. Theluthi mbili ya wajumbe inaruhusu kufanyika kwa mkutano.
3.      Mkurugenzi Mkuu ndiye atakuwa mwenyekiti wa kikao

MAJUKUMU YA MKUTANO MKUU

a.      Mkutano mkuu ni kikao chenye maamuzi ya mwisho kwa shughuli zote za kikundi.
b.      Kitakuwa ndicho kikao cha kuchagua viongozi wa kikundi na kuidhinisha Bodi ya wadhamini.
c.       Mkutano mkuu utapitisha bajeti ya kikundi na una mamlaka ya kufanya marekebisho ya viwango vya michango ya kikundi.
d.      Kikao kitapokea na kujadili taarifa ya mapato na matumizi kutoka bodi ya wakurugenzi.
e.      Mkutano mkuu ndicho kikao chenye mamlaka ya kurekebisha au kubadili katiba  kwa kadri itakavyofaa kulingana na mahitaji ya kikudi ya wakati huo.
f.        Mkutano mkuu ni kikao kinachotengeneza sera, taratibu na miongozo ya uendeshaji wa kikundi na kutoa maagizo kwa bodi ya wakurugenzi kwa ajili ya utekelezaji.


  1. BODI YA WAKURUGENZI
1.      Bodi ya Wakurugenzi ni kikao kitakachoundwa na wakurugenzi wote sita (6) wa kikundi pamoja na wajumbe wawili watakaochaguliwa na mkutano mkuu.
2.      Kikao kitafanyika mara moja kila baada ya miezi miwili (2). Theluthi mbili ya wajumbe itaruhusu kufanyika kwa kikao.
3.      Mkurugenzi Mkuu ndiye atakuwa mwenyekiti wa kikao.

MAJUKUMU YA BODI YA WAKURUGENZI

a.      Bodi ya Wakurugenzi ni kikao kitakachosimamia na kuratibu shughuli zote za kila siku za kikundi. Itasimamia utekelezaji wa maagizo yote ya mkutano mkuu
b.      Kikao kitapokea na kujadili taarifa ya mapato na matumizi ya fedha za kikundi na kuwasilisha taarifa hiyo katika mkutano mkuu.
c.       Bodi itaratibu shughuli zote za uchaguzi za kikundi ikiwa ni pamoja na kuteua Bodi ya wadhamini na wasaidizi wa mkurugenzi wa muziki.
d.      Kikao kitakuwa na majukumu ya kuidhinisha matumizi yo yote ya fedha ndani ya kikundi.
e.      Bodi itapokea, itajadili na kuratibu mabadiliko ya katiba na kupitisha maombi ya wanachama wapya.
f.        Bodi ya Wakurugenzi ina wajibu wa kupokea na kujadili taarifa ya tabia na mienendo isiyo ya kumtukuza Mungu itakayofanywa na viongozi au wanachama kabla ya kufikisha mapendekezo ya taarifa hiyo katika mkutano mkuu kwa ajili ya maamuzi. 

  1. BARAZA LA WADHAMINI
1.       Baraza la wadhamini itaundwa na wajumbe watatu watakaoteuliwa na Bodi ya wakurugenzi. Mkurugenzi mkuu atakuwa mjumbe mwalikwa.
2.      Baraza itafanya kikao kimoja kila mwaka. Mwenyekiti wa kikao atachaguliwa miongoni mwa wajumbe.

MAJUKUMU YA BODI YA WADHAMINI

a.      Kusimamia misingi yote ya kanisa na kikundi na kuhakikisha kuwa inafuatwa
b.      Kudhamini shughuli zote za kikundi ikiwa ni pamoja na ziara na mialiko, pia kushiriki kukitafutia kikundi ufadhili.



SEHEMU YA VII

UCHAGUZI

Mkutano mkuu wa uchaguzi utafanyika kila baada ya miaka mitatu (3). Uchaguzi wa dharura unaweza kuitishwa muda wowote ili kuziba nafasi inayoweza kuachwa wazi kutokana na ukomo wa uongozi kama inavyofafanuliwa katika sehemu ya VIII ya katiba hii. Shughuli za uchaguzi ndani ya kikundi zitazingatia utaratibu ufuatao:
  1. Bodi ya Wakurugenzi itakuwa na mamlaka ya kufanya uteuzi wa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ambaye kwa mujibu wa matakwa ya katiba hii atatoka nje ya kikundi. Huyu aweza kuwa mzee wa kanisa, mchungaji wa ngazi ya mtaani au Conference kwa kadri ambavyo bodi itaona anafaa.
  2. Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi atapendekeza majina mawili (2) ya wajumbe wa Tume yake ambao waweza kutoka ndani au nje ya kikundi ambao si miongoni mwa viongozi wanaomaliza muda wao. Majina hayo yatawasilishwa kwenye kikao cha Bodi ya Wakurugenzi kwa ajili ya uthibitisho.
  3. Tume ya uchaguzi itaundwa mwezi mmoja kabla ya siku ya uchaguzi..
  4. Wanachama watakaoomba kuchaguliwa watapaswa kujaza fomu maalumu za maombi zitakazoandaliwa na Tume ya Uchaguzi. Fomu zitaonyesha nafasi ya uongozi.
  5. Viongozi waliomaliza muda wao wanaruhusiwa kujaza fomu za maombi. Hakuna kipindi maalumu cha ukomo wa uongozi hadi katiba hii itakapofanyiwa marekebisho.
  6. Nafasi za uchaguzi ni:
a.      Mkurugenzi Mkuu
b.      Kaimu Mkurugenzi Mkuu
c.       Katibu Mtendaji
d.      Mkurugenzi wa Fedha
e.      Mkurugenzi wa Maktaba na Mawasiliano
Nafasi ya Mkurugenzi wa Kwaya na Mahusiano ni ya kitaaluma. Mkurugenzi atateuliwa na Bodi ya Wakurugenzi.
  1. Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi atapanga tarehe na muda wa kufanya uchaguzi. Atapanga utaratibu ufuatao ili kurahisisha zoezi zima la uchaguzi:
a.      Wagombea wote lazima watajwe kwa nafasi wanazogombea. Kila mgombea atapewa fursa ya kujitambulisha na kueleza kwa nini anafaa kuchaguliwa kwa nafasi anayoiomba.
b.      Utaratibu wa uchaguzi ni wa kura ya siri na Mwenyekiti atazingatia mpango maalumu kama ilivyoonyeshwa katika kipengele nambari 6 hapo juu.
c.       Nafasi yenye mgombea mmoja, Mwenyekiti wa Tume atamtangaza kuwa mshindi moja kwa moja baada ya kupigiwa kura ya NDIYO.
d.      Kwa nafasi yenye wagombea zaidi ya mmoja, mshindi atapatikana kwa wingi wa kura zaidi ya wagombea wenzake.
  1. Kadri ya 75% ya mahudhurio ya wanachama itaruhusu kufanyika uchaguzi.
  2. Matokeo ya uchaguzi yatatangazwa na Mwenyekiti wa Tume na ndiyo yatakuwa matokeo ya mwisho.





SEHEMU YA VIII

UKOMO WA UONGOZI NA UANACHAMA

Tunalenga kuhakikisha kwamba kila kiongozi na mwanachama anajiimarisha na kusimama katika misingi ya imani na kutimiza malengo yote ya kikundi kama ilivyoelezwa katika sehemu ya II na III ya katiba hii. Kushindwa kukidhi matakwa ya misingi na malengo ya kikundi kutasababisha ukomo wa uongozi au uanachama kama inavyofafanuliwa hapa chini:
  1. UKOMO WA UONGOZI
1.      Kipindi cha uongozi ni miaka mitatu. Endapo kiongozi hatochaguliwa tena kurudia madaraka yake uongozi wake utakuwa umekoma.
2.      Ukomo wa uongozi utafika endapo kiongozi aliyepo madarakani atajiuzulu kwa ridhaa yake, kufutwa uanachama au kusimamishwa uongozi kwa manufaa ya kikundi.
3.      Ukomo wa uongozi utafika endapo kiongozi aliyeko madarakani atahama au kuaga dunia (kifo).
  1. UKOMO WA UANACHAMA
1.      Ukomo wa uanachama utafika endapo mwanachama atajiuzulu uanachama kwa ridhaa yake au kuachishwa uananchama kwa makosa yake.
2.      Uanachama utakoma endapo mwanachama atashindwa kulipa ada na michango mingine iliyoamriwa na kikundi kwa vipindi vitatu mfululizo.
3.      Kifo, uhamisho na kushindwa kuhudhuria vikao mara tatu mfululizo ni miongoni mwa vigezo vinavyotumika katika ukomo wa uanachama.





SEHEMU YA IX

MAPATO YA KIKUNDI

Kikundi kinatarajia kukusanya mapato yake kutoka vyanzo mabalimbali kama ilivyoorodheshwa hapa chini:
  1. Fedha za kiingilio (Tshs. 5,000/=) na Ada za uanachama kwa mwaka (Tshs. 10,000/=)  
  2. Michango mbalimbali ya wanachama.
  3. Michango ya wahisani na wadau mbalimbali.
  4. Harambee na uzinduzi wa albamu za kwaya.
  5. Mauzo ya kanda na CD’s.
  6. Mikopo toka taasisi mbalimbali za fedha.
  7. Miradi itakayoanzishwa na kikundi.
Kikundi kina maono ya kutumia makusanyo yake katika mambo yafuatayo:
  1. Kulipa Zaka na Sadaka.
  2. Kuchangia katika shughuli za maendeleo ya kanisa k.v. huduma za injili, afya, elimu na ujenzi.
  3. Kutoa huduma ya msaada kwa watu wenye uhitaji walio ndani na nje ya kanisa.
  4. Kuhudumia na kuendesha shughuli mbalimbali za kikundi.
  5. Kutoa msaada wa kimahitaji kwa matatizo yatakayowakabili wanachama.
NYONGEZA:       
  1. Kikundi kitafungua na kumiliki Akaunti katika Benki ya CRDB tawi la Musoma.
  2. Katiba inatambua watia sahihi watatu (3) kwa nyadhifa zao kama ifuatavyo:
a.      Katibu Mtendaji…………………………………Mtia sahihi mkuu.
b.      Mkurugenzi wa Fedha
c.       Mjumbe mmoja toka Bodi ya Wakurugenzi.
  1. Wajumbe wawili kati ya hao watatu, Sahihi ya Katibu Mtendaji ikiwa ya lazima, wanaruhusiwa kutoa pesa Benki.


SEHEMU YA X

MAREKEBISHO YA KATIBA

  1. Katiba hii imeandaliwa kwa kusudio la kukidhi haja na mahitaji ya kikudi. Iwapo itashindwa kufikia malengo hayo kwa kipindi au mazingira muafaka, Bodi ya Wakurugenzi itawajibika kuifanyia marekebisho kabla ya kuifikisha Mkutano Mkuu kwa maamuzi ya mwisho.
  2. Mwanchama yeyote aweza kuleta hoja ya mabadiliko mbele ya Bodi ya Wakurugenzi kwa ajili kupitia na kufanyia marekebisho.
  3. Siku ya tukio la marekebisho, kwaya itapendekeza mwakilishi mmoja atakayeungana na Bodi katika kikao husika. Marekebisho yaweza kufanywa kwa njia ya kura pale muafaka unaposhindwa kufikiwa.
  4. Marekebisho ya katiba hayatokuwa halali hadi nakala ya marekebisho hayo itakapopitishwa na 75% ya kura za mkutano mkuu chini ya ushauri wa Mwanasheria atakayependekezwa na Bodi ya Wakurugenzi.
  5. Marekebisho ya katiba yatafanyika mara moja katika kipindi cha miaka mitatu au pale ambapo itapoonekana inafaa kulingana na mahitaji ya kikundi.










ANDIKO HILI LIMEANDALIWA NA KUIDHINISHWA LEO JUMAMOSI, TAREHE 20 JULAI, 2013

BODI YA WAKURUGENZI:                                                                                                                 
Na.
Jina
Sahihi
Cheo
1
Mkama L. Rugina

Mkurugenzi Mkuu
2
Fredy N. Jeje

Kaimu Mkurugenzi Mkuu
3
Emmy Msiba

Katibu Mtendaji
4
Bethy Msiba

Mkurugenzi wa Uchumi na Fedha
5
Gaya Masatu

Mkurugenzi wa Maktaba na Mawasiliano
6
Akiba Mashenene

Mkurugenzi wa Muziki na Mahusiano
7
Phoebe Yonah

Mjumbe
8
David Mayunga

Mjumbe






1 comment:

Anonymous said...

Kazi nzuri, hongereni sana